پایگاه اطلاع رسانی آیت الله ابراهیم امینی قدس سره

Matarajio Mabaya

 

Mpendwa Bibi! Wewe ni mwanamke mkuu wa familia yako. Uwe na hekima na uweledi. Panga vizuri matumizi yako. Panga bajeti ya matumizi yako kwa njia ambayo haitasababisha hasara kwa utajiri na hekima yako.

Usishindane na wengine na uwaonee wivu. Kama unaona nguo nzuri imevaliwa na mwanamke, au kama unavutiwa na fanicha na vyombo ambavyo umeviona kwenye nyumba ya rafiki, usimlazimishe mumeo kununua vitu kama hivyo ambavyo vinazidi uwezo wake wa kifedha na pengine atalazimika kukopa. Je, si vema zaidi kungoja hadi hapo ambapo hali ya kipato itaruhusu au itakapopatikana akiba ya ziada ya kuwezesha kununua vitu visivyo vya muhimu?

Mara nyingi ni wale wanawake wajinga na wanaojipendelea ambao hushindwa, na kuwa wabadhirifu na kutaka kushindana. Wanawake wa aina hii huwalazimisha waume zao kuingia kwenye madeni na huchoshwa na kukasirishwa na kujaribu kuridhisha matakwa yao yasiyo weza kutoshelezwa. Wakati mwingine, ufumbuzi wa aina moja tu uliopo kwa wanaume wa kutatua matatizo haya ni uamuzi wa kumtaliki mke au kujiua.

Wanawake ambao hawatambui madhumuni ya kweli na maana ya ndoa na badala yake wanaifikiria kama utumwa ambapo mwanamume anapatikana kwa lengo la kutimiza matamanio yao ya kitoto na mahitaji ya kiulimwengu.

Wanawake wa namna hii wanataka mume ambaye atawahudumia kama mtumwa na hawatapinga njia zao za matumizi. Wanawake wa aina hii mara nyingine huenda mbali zaidi. Wanawafanya waume zao watumie zaidi ya uwezo wao hali ambayo inaweza kuwafilisi, wanaweza kufanya mauaji au matokeo yoyote ya msiba.

Wanawake wa aina hii ni aibu kwa wanawake wenzao. Endapo matarajio yake makubwa yanasababishwa kutalikiana, mwanamke atanyang’anywa mapenzi ya watoto wake na ataishi maisha ya upweke.

Kwa wanawake wa aina hii si rahisi kuolewa tena kwa urahisi. Hata kama inatokea, hakuna uhakika wa ndoa ya pili kama itadumu, kwani binadamu wengi hawapendi kuwekwa katika utumwa. Na mume mpya inawezekana naye asiwe na uwezo wa kutimiza mahitaji yao kabisa kuliko hata wa mwanzo.

Mpendwa Bibi! Badala ya kuwa mwenye tamaa sana, jaribu kuwa mwenye busara. Tumia muda mwingi na juhudi kwa ajili ya ustawi wa familia yako na mumeo badala ya kujaribu kuiga mambo ya kila mtu. Kama mumeo anaumia kupita kiasi, mzuie na udhibiti matumizi yake yasiyo ya muhimu. Badala ya kununua bidhaa zisizo za muhimu, ni vema kuweka kiasi fulani cha akiba kwa ajili ya matatizo ya siku za usoni.

Katika hadith Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke yeyote ambaye halingani na mume wake na humshawishi afanye mambo zaidi ya uwezo wake, basi matendo yake hayatakubaliwa na Mwenyezi Mungu, ataonja ghadhabu ya Mwenyezi Mungu mnamo Siku ya Ufufuo.”

Katika hadith nyingine, Mtukufu Mtume (s.a.w.w) alisema: “Mwanamke yeyote asiyelingana na mumewe, haridhiki na kile ambacho Mwenyezi Mungu amewajaalia na humtendea mume wake ubaya kwa kudai ampe zaidi ya uwezo wake, basi matendo yake (au ibada ya mke) hayakubaliki kwa Mwenyezi Mungu na Atamkasirikia mwanamke huyo.”

Katika hadith nyingine, Mtume (s.a.w.w) alisema: “Baada ya kumwamini Mwenyezi Mungu, hapana neema iliyo kubwa zaidi ya kuwa na mume au mke mnayeelewana naye.”